Waziri wa kilimo Mutahi Kagwe, ametoa makataa ya mwezi mmoja kwa wahifadhi wa mahindi kuingiza sokoni akionya kuwa kutofanya hivyo kutailazimu serikali kuruhusu uagizaji wa mahindi bila ushuru ili kuleta utulivu wa gharama ya unga wa mahindi.

Akiwahutubia wakulima katika bodi ya kitaifa ya nafaka na mazao ya Sagana (NCPB), Kagwe alisema kipaumbele cha serikali inabaki kununua mahindi kutoka kwa wakulima wa ndani ili kujaza hifadhi ya kitaifa ya chakula, lakini akatahadharisha kuwa uagizaji kutoka nje hautaepukika ikiwa akiba ya kutosha haitatolewa ndani ya siku 30.

kulingana na waziri huyo, serikali inalenga ununuzi wa mara moja wa angalau magunia milioni moja na laki saba ya mahindi, kwa lengo la muda mrefu la kuhifadhi magunia milioni nne katika hifadhi ya nafaka. hata hivyo, ni magunia 186,000 pekee ambayo yamewasilishwa kufikia sasa, upungufu ambao ulihusishwa na uhifadhi na desturi za kubahatisha huku hali ya ukame ikianza kujitokeza katika baadhi ya maeneo ya nchi.