Gavana wa Nandi, Stephen Sang, ameikosoa vikali bodi ya utumishi kwenye kaunti yake, akidai kuwa baadhi ya maafisa wake wamekuwa wakiitisha hongo ili kuwaajiri wafanyikazi na kuzuia juhudi za kuwarejesha kazini wafanyakazi walioondolewa kwenye orodha ya malipo.
Sang amesema mchakato wa kuajiri wafanyakazi ulilenga kuwapa kipaumbele wale walioathirika na kuondolewa kwenye mfumo wa malipo kabla ya kutoa nafasi zingine
Aidha ameishutumu bodi hiyo kwa madai ya kushirikiana na baadhi ya wanaowania nyadhifa za kisiasa, akisema njama hiyo inalenga kuvuruga mchakato wa ajira na kuingiza siasa katika mageuzi muhimu ya kaunti.
Sang ametaja pia uboreshaji wa maslahi na masharti ya kazi kwa walimu wa ECDE kama mojawapo ya mageuzi anayosema yanakabiliwa na changamoto za kisiasa,akitaka mchakato wa utumishi wa umma uendeshwe kwa uwazi, haki na kwa kuzingatia maslahi ya wafanyakazi.

